VITA dhidi ya biashara ya
madawa ya kulevya ni ngumu sana, dirisha la mafanikio ya kudhibiti
linafungwa na vigogo wauza unga ambao wana fedha nyingi zinazoyumbisha
sheria kuchukua mkondo wake.
Pointi nambari moja ni
uwepo wa ripoti za ukamatwaji wauza unga lakini hukumu hazitolewi, swali
kwa nini hawahukumiwi likipashwa moto ili kuunguza mamlaka
zinazohusika, Uwazi linafichua siri nzito kuhusu madai ya vigogo
waliokamatwa na kuachiwa.
Watu wanne ambao wanatajwa kuwa miongoni mwa vinara wa madawa ya
kulevya nchini, walikamatwa na madawa ya kulevya yenye thamani ya
shilingi bilioni 6.2 kisha wakafikishwa mahakamani ambako inadaiwa
wameachiwa katika mazingira tatanishi.
Vigogo hao wanne, wapo
Watanzania wawili na wengine ni raia wa Pakistan ambao sasa hivi
inadaiwa wameshatoroka kwenda nje ya nchi.
Februari 21, 2011, jeshi
la polisi kupitia kitengo cha kudhibiti na kupambana na madawa ya
kulevya, kiliwakamata wafanyabiashara hao ambao majina yao ni William
Chonde na Kambi Zuberi (Watanzania) pamoja na Wapakistan, Abdul Ghan
Peer Bux na Shahbaz Malk.
Watu hao, walikamatwa na mzigo huo Mbezi Jogoo, Dar es Salaam kwenye
nyumba ya Chonde, wakiwa na madawa ya kulevya aina ya heroine, yenye
uzito wa kilo 179 ambayo thamani yake ni shilingi 6,265,000,000.
Sera ya Uwazi ni
kuendeleza safari iliyoianzisha kwa vile ndilo liliandika pale
walipokamatwa zaidi ya miaka miwili iliyopita. Wiki mbili zilizopita,
lilianza upekuzi kujua kesi hiyo imefikia wapi.
Uchunguzi wa waandishi
wetu uliweza kubaini kuwa watuhumiwa hao wa madawa ya kulevya waliachiwa
na mahakama kuu kwa dhamana, kinyume na sheria ya madawa ya kulevya
inavyoeleza.
Sheria ya madawa ya
kulevya ya mwaka 1996, sura ya 95, kipengele nambari 9, kifungu nambari
27, kifungu kidogo nambari 1A, kinasema: “Yeyote atakayekamatwa na
madawa ya kulevya yenye thamani zaidi ya shilingi milioni 10 hapaswi
kupewa dhamana.”
Vilevile, sheria hiyo
inaendelea katika kifungu kidogo nambari 1B ambacho kinasema: “Yeyote
atakayekamatwa akisafirisha madawa ya kulevya hapaswi kudhaminiwa.”
Mkuu wa Kitengo cha
Kudhibiti na Kupambana na Madawa ya Kulevya Tanzania, Godfrey Nzowa,
alipoulizwa kuhusu kile anachokifahamu kufuatia kuachiwa kwa watuhumiwa
hao, alijibu:
“Mimi sijui, waliachiwa
mahakamani. Kazi yetu sisi ilikuwa ni kuwakamata, kila kitu kikapelekwa
kwa DPP (mkurugenzi wa mashtaka), baada ya hapo kesi ilikwenda kwa
msajili wa mahakama.
“Nijuavyo mimi ni kwamba walifikishwa mahakamani na nilisikia waliachiwa kwa dhamana,” alisema Nzowa.
Yapo madai kwamba baada
ya watuhumiwa hao kupewa dhamana, walikabidhiwa hati za kusafiria
(passport) ambazo ziliwawezesha kutoroka. Uwazi lambana Nzowa;
MWANDISHI: Unaweza kufahamu kigezo kipi kilitumika kuwapa dhamana watuhumiwa hao? Maana sheria inakataza.
NZOWA: Nadhani mahakama ndiyo inapaswa kuulizwa swali hilo. Siwezi kuisemea, maana ule ni mhimili mwingine huru.
MWANDISHI: Inadaiwa wewe ndiye uliwapa passport zao na sasa tunaambiwa walishatoroka nchini, hili limekaaje?
NZOWA: Ni kweli tuliwapa passport zao, tuliagizwa na mahakama kufanya hivyo.
Msajili wa Mahakama Kuu,
Benedict Mwingwa, alipoulizwa kuhusu kuachiwa kwa watuhumiwa hao kwa
dhamana, aling’aka, kisha akaahidi kufuatilia kujua kisa na mkasa.
“Nimeshtushwa sana na
hilo jambo. Ni kweli sheria inakataza, sasa watuhumiwa kama hao
hawakupaswa kudhaminiwa. Nalifanyia kazi, nitakutana na jaji
anayesikiliza kesi hiyo aniambie sheria aliyotumia,” alisema Mwingwa.
Uchunguzi uliofanywa
umebaini kwamba baada ya malalamiko ya muda mrefu kuhusu kusuasua kwa
kesi za madawa ya kulevya ambayo yanaelekezwa Mahakama Kuu, Jaji
Kiongozi, Fakhi Jundu, aliitisha mkutano wa dharura wiki mbili
zilizopita.
Mkutano huo ulishirikisha
majaji wa mahakama kuu, idara ya usalama wa taifa, Takukuru, ofisi ya
DPP, mkemia mkuu wa serikali, magereza, polisi na kitengo cha kudhibiti
na kupambana na madawa ya kulevya.
Vyanzo vyetu vinasema
kuwa katika mkutano huo, maazimio ya pamoja ni kila idara kutimiza
wajibu wake bila kutazama sura wala nafasi ya mtu ili haki ionekane
ikitendeka, huku ikisisitizwa kesi kuharakishwa na hukumu kutolewa.
No comments:
Post a Comment