Pages

Translate

Friday 31 January 2014

AIBA MTOTO WA MWEZI MMJO NA KUTOROKA NAE

MKAZI wa Bunju B, Grace Chapanga(34), anashikiliwa na Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam kwa tuhuma za wizi wa mtoto mchanga wa kike mwenye umri wa mwezi mmoja. 


Kamanda wa Kanda hiyo, Kamishna wa Polisi Suleiman Kova alisema Chapanga alimuiba mtoto huyo, Veis Venus Desemba 27 mwaka jana katika maeneo ya Mwenge jijini Dar es Salaam.

Alisema mtuhumiwa huyo alitenda kosa hilo baada ya kumhadaa mama wa mtoto aitwae Salma Frank (29), mkazi wa Kawe Mji Mpya kwa kumuomba ambebee huku wote wakiwa abiria wa daladala, wakitokea Hospitali ya Mwananyamala.

Kova alisema walipofika kituo cha daladala Mwenge, mtuhumiwa aliteremka upesi na kutoweka na mtoto, wakati mwenye mtoto akikusanya vitu vingine alivyokuwa navyo.

“Chapanga alitenda kosa hilo kwa kushirikiana na Halima Alabi (46), mkazi wa Boko Maliasili ambaye naye alikamatwa Januari 4 mwaka huu,” alisema.

Alisema watuhumiwa wote baada ya kutenda kosa hilo, waliondoka kwenda Sumbawanga mkoani Rukwa, ambapo Chapanga alimdanganya mumewe kuwa yeye ni mjamzito na angependa kwenda kujifungulia nyumbani kwao Sumbawanga.

“Upelelezi wa tukio hilo ulifanikisha kumkamata mume wa Chapanga aitwaye Daniael Mwaikambo (38), mkazi wa Bunju B, ambaye pia ni mfanyakazi wa Uhamiaji Makao Makuu Dar es Salaam na kwenda naye Sumbawanga, ambapo walimkuta mtuhumiwa na kumkamata” alisema.

Inasemekana kwamba tangu Chapanga na Mwaikambo wafunge ndoa mwaka 2010 hadi sasa, wanandoa hao hawajabahatika kupata mtoto.

Aidha, Kova alisema mwaka 2012 Chapanga alifanyiwa upasuaji wa uvimbe tumboni na daktari alimwambia hatoweza kushika mimba tena, jambo ambalo mwanamke huyo hakumueleza ukweli mume wake wala ndugu yake yeyote hadi alipopanga njama na hatimaye kufanikiwa kumuiba mtoto huyo.

Alisema upelelezi wa shauri hilo unaendelea kwa kufuatilia uchunguzi wa vinasaba (DNA) vya mama mzazi, mtuhumiwa na mtoto aliyeibwa. Pia alisema mtoto huyo amekabidhiwa kwa mama yake mzazi. HABARILEO

No comments:

Post a Comment