Pages

Translate

Thursday 12 December 2013

MSIGWA ASISITIZA KUWA BARAZA LA MAWAZIRI LIMEDUMAA

  
MBUNGE wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa (CHADEMA), amesema asilimia 40 ya Baraza la Mawaziri limedumaa kwa sababu limeshindwa kutekeleza majukumu yake. Msigwa pia alikilaumu Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwa kimeshakuwa chakavu kwa kushindwa kutoa matumaini kwa Watanzania. Alitoa kauli hiyo bungeni juzi wakati akichangia mjadala wa taarifa za Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa, Kamati ya Bunge ya Bajeti na Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali. Alisema kila mwaka wabunge wamekuwa wakizungumza mambo yale yale na serikali imekuwa ikijibu vilevile wakati matatizo yale yale yameendelea kuwepo.

      “Bunge la mwaka juzi la Bajeti nilitoa takwimu za Wizara ya Afya, kwamba asilimia 42 ya watoto wanaozaliwa Tanzania wamedumaa, mtu anayedumaa hawezi kufikiri, hawezi kuhoji wala kudadisi, kwa kutumia takwimu hizi hizi Baraza la Mawaziri  ambao ni zaidi ya mawaziri 56, asilimia 40 wamedumaa na moja ya sababu ya kudumaa ni changamoto wanazozipata katika Bunge hili. “Kila mwaka tunazungumza yale yale, tunapata majibu yale, watu hawabadiliki maana yake kuna tatizo kwenye akili zao. “Matatizo ya wizi wa fedha lazima tuyapatie ufumbuzi, haiwezekani kila siku tuseme yale yale, matatizo yapo pale pale,” alisema. Mchungaji Msigwa alisema lazima kuwepo kwa nidhamu ya  matumizi ya fedha za serikali na kuitaka serikali kuzikumbusha halmashauri kwamba nchi inaongozwa kwa mfumo wa vyama vingi.
        “Katika jimbo langu magari ya halmashaiuri yanatumika katika shughuli za chama, mkurugenzi na meya wanalazimishwa  na madiwani kwenda uwanja wa ndege kumpokea Nape na Kinana, huu ni utovu wa nidhamu wa matumizi ya fedha za umma na haukubaliki. “Ukiona mbunge rafiki wa  mkurugenzi uje hapo kuna ‘deal’, ukiona meya rafiki wa mkurugenzi hapo kuna kitu. Mkurugenzi na mbunge wakiwa maaadui ujue  mkurugenzi huyo anasimamia vizuri matumizi ya fedha,” alisema. Msigwa alisema ni wakati muafaka wa Watanzania kuchagua chama mbadala kuongoza nchi badala ya kuendelea  kuichagua CCM. “Nashukuru sasa hadi Katibu Mkuu wenu wa chama kasema wazi kwamba baadhi ya mawaziri ni mzigo, kazi yao ni kufunga tai na kutembea mjini tu.

      “Mbeya aliwaomba radhi Watanzania, sasa mnaanza kuongea lugha yetu kwamba kuna mizigo, yaani hadi muambiane wenyewe ndo mnakubaliana… Hii Big Result Now mmewakaririsha watu kama kasuku, mnahadaa Watanzania wakati watu ni wale wale, wanafikiri vilevile, wanatenda vile vile eti Big Result Now. “Watanzania muda muafaka umefika, hiki chama chakavu kimechoka ni vizuri tulete chama mbadala, mabadiliko yamefanywa sana hasa katika Baraza la Mawaziri, lakini mambo bado yale yale,” alisema. Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi (CHADEMA) alisema chanzo kikubwa cha ubadhirifu wa fedha katika halmashauri ni wakurugenzi na wenyeviti wa halmashauri au mameya huku akitoa mfano kwa Jiji la Mbeya. Mbunge wa Busega, Dk. Titus Kamani (CCM) aliitaka serikali kuchukua hatua za haraka kwa wale wote watakaobainika kuiba fedha za serikali. Dk. Kamani pia alimtetea Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kwamba ni kiongozi muadilifu, na kwamba anashangaa siasa za Tanzania kiongozi muadilifu ndiye anayepigwa mawe.

No comments:

Post a Comment