Kijana Said Hassan anadaiwa kumuua kikatili mtoto wa dada yake, Fatihia ‘Fety’ Said (2) na kuibua simanzi nzito.
Tukio hilo la kinyama lilitokea hivi karibuni maeneo ya Keko-Tolori jijini Dar ambapo ilidaiwa kuwa jamaa huyo ni teja.
Akizungumza kwa uchungu, mama wa Fatihia alisema kuwa siku ya tukio 
(Jumatano iliyopita) aliamka asubuhi salama na mtoto wake ambapo 
ilipofika muda wa saa 2:00 asubuhi alimpa mwanaye chai akawa anakunywa 
huku anatembea, wakati huo yeye alikuwa akifanya kazi zake za usafi wa 
ndani.
“Nilipomaliza usafi na kazi zangu nikaanza kumtafuta mtoto, sikumuona, 
niliingiwa na hofu hivyo nikawa namsaka kila kona ya nyumba lakini 
sikumuona.
“Nilikwenda nyumba ya jirani ambapo ndiko huwa anakwenda mara nyingi 
kucheza lakini pia sikumkuta, baada ya kujiridhisha kuwa hayupo nilienda
 kutoa matangazo msikitini kuwa mtoto amepotea,” alisema Mwamvita 
Hassan, mama wa mtoto huyo.
Alisema kuwa baada ya jitihada zote hizo bila mwanaye kupatikana 
aliondoka na wenzake na kwenda Mbagala, Dar akihisi labda kuna mtu 
amemchukua mtoto wake kwani huko kuna nyumba yao nyingine lakini nako 
hawakumkuta.
Kwa mujibu wa bibi wa mama Fatihia, walipomuuliza mtoto wa jirani 
alisema kuwa amemsikia mtoto akilia chumbani kwa mjomba’ke Said waende 
wakaangalie huenda alikuwa huko.
“Kweli tulivyoangalia tulimkuta mtoto amewekewa nguo chini ya kitanda, 
juu yake kawekewa magodoro, tayari alishaaga dunia, hatukujua kama 
alimnyonga au alimfanya nini kwani bado uchunguzi unafanyika kwa sababu 
mtoto alikutwa na mapovu mdomoni,” alisema bibi huyo.
Mjomba wa mtuhumiwa, Shaban Juma alisema kuwa mtuhumiwa hakuwa na akili 
nzuri kwani mara nyingi amekuwa akimpeleka Hospitali ya Wilaya ya 
Temeke, Dar na akawa anapewa dawa ingawa yeye hakutambua ni dawa gani.
Mjomba huyo alipoulizwa kama mtuhumiwa alikuwa akitumia madawa ya 
kulevya, alikubali na kusema kuwa kuna mtu alimthibitishia kuwa amekuwa 
akimuona ‘akijidunga’.
Habari za uchunguzi zilibainisha kuwa mtuhumiwa huyo amewahi kufanya 
matukio mbalimbali kama kujaribu kuchoma nyumba yao, kukojolea maji ya 
kunywa na kutishia kufanya kitu cha ajabu ambacho watu hawatakisahahu.
Baba wa mtoto aliyejitambulisha kwa jina moja la Said alisema kuwa 
alisikitishwa na tukio lililompata mtoto wake lakini huyo shemeji yake 
alikuwa akimtishia kila siku. 
“Nimeumia sana lakini naacha sheria ichukue mkondo wake kwa sababu ameshakamatwa,” alisema.
 

 
No comments:
Post a Comment