Pages

Translate

Thursday 15 August 2013

WAKAZI WA ARUSHA WAACHWA MIDOMO WAZI PESA ZILIZOTUMIWA MAZISHI YA MSUYA






MAZISHI ya kufuru ya yule bilionea mfanyabiashara wa madini ya tanzanite mkoani hapa, marehemu Erasto Saimon Msuya, yameacha gumzo kubwa.
Mfanyabiashara huyo aliuawa kwa kumiminiwa risasi zaidi ya 20 na watu wawili wasiojulikana Agosti 7, mwaka huu maeneo ya Kia wilayani Hai, Kilimanjaro kabla ya kupumzishwa Jumanne wiki hii kijijini kwao Kairo huko Simanjiro mkoani Manyara.

Baada ya kutokea kwa mauaji hayo, iliundwa kamati ya mazishi ikihusisha  wafanyabiashara wa madini ya tanzanite pekee ambayo ilitengeneza bajeti ya maziko ya tak
ribani shilingi milioni 100.
Habari kutoka ndani ya kamati hiyo zilieleza kuwa gari maalum la kifahari na jeneza lililobeba mwili vilinunuliwa Nairobi nchini Kenya.
Jeneza lake


INASEMEKANA kuwa jeneza hilo liliagizwa na kampuni inayojishughulisha na shughuli za maziko ya Montezuma & Monalisa Funeral Home.
Ilielezwa kuwa jeneza hilo lilinunuliwa shilingi milioni nane ikidaiwa kuwa lilikuwa lina uwezo wa kufunga na kufunguliwa kwa kutumia ‘rimoti’.
IMG-20130812-WA0011

Ilidaiwa kuwa jeneza hilo lilikuwa na vishikio maalum vilivyokuwa viking’aa kama dhahabu au tanzanite na kulifanya kuonekana la aina yake.
Hali hiyo iliwaacha na mshangao maelfu ya waombolezaji waliofika kuaga mwili wakati wa ibada iliyofanyika nyumbani kwa marehemu, maeneo ya Kwaiddi, barabara inayoelekea Ngaramtoni wilayani Arumeru kabla ya kusafirishwa kwenda Simanjiro kwa maziko.
Pamoja na lile lililobeba mwili wa marehemu, msafara wa magari ya kifahari kuelekea kijijini huko ulisababisha Jiji la Arusha kuzizima kwa majonzi huku wengi wakishindwa kuamini kama jamaa huyo amefariki dunia na kuacha utajiri wa kutisha.
“Hebu ona, hakuna gari la ovyo, yote ni makali. Ingekuwa utajiri unaweza kumfufua mtu, basi Erasto angefufuliwa,” alisema mmoja wa waombolezaji akimwelezea jamaa huyo kuwa alikuwa mtu ‘smati’.
Habari za ndani zilidai kuwa hata suti aliyozikwa nayo ilitoka nje ya nchi, London, Uingereza kwa Malkia Elizabeth.
Pia ilidaiwa kuwa jamaa huyo alizikwa na cheni ya dhahabu (gold) shingoni yenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 10.
Habari zilinyetisha kuwa huduma kama vyakula, vinywaji, mapambo na magari ya kukodishwa kutoka Arusha kwenda kijijini na kurudi viligharimu zaidi ya shilingi milioni 80.
Ili kuthibitisha kuwa msiba huo haukuwa wa kitoto, Msema Chochote ‘MC’ alikuwa ni staa mkubwa wa filamu za Kibongo, Jacob Steven ‘JB’.
Habari zilidai kuwa waombolezaji walipofika kijijini kwa ajili ya maziko Jumanne mchana, watu walikanyagana makaburini huku vijana wakitaka azikwe na mtu hai wa kumlinda.
Walipofika walikuta kaburi la kifahari limeshajengwa ambapo kulikuwa na zulia maalum la kufuta miguu kabla ya kukanyaga marumaru za madini ya tanzanite zilizolizunguka.
Kuthibitisha kuwa ilikuwa ni kufuru, baadhi ya wachimbaji wadogo ‘nyoka’ walikuwa wakiwataka matajiri kulifungia kaburi hilo umeme na kiyoyozi. 
Kujengwa mnara wa kumbukumbu





Baada ya mazishi hayo, inaelezwa kuwa familia ilikubaliana kufanya juu chini kulinunua shamba alilouliwa katika Mji wa Bomang’ombe, Mtaa wa Wasomali eneo la Mjohoroni wilayani Hai, Kilimanjaro ili kujenga mnara wa kumbukumbu.
Ilidaiwa kuwa baada ya kujenga mnara huo, familia itakuwa inatembelea eneo hilo Agosti 7, kila mwaka kwa ajili ya tambiko.
Kaka wa marehemu, Israel Msuya, alisema kuwa walifikia uamuzi wa kufanya mazishi hayo kwenye makaburi ya familia ya mzee Elisaria Msuya ‘Kikaango’ ambaye ni baba wa marehemu Erasto.
Kwa mujibu wa kaka huyo wa marehemu, familia haitalipiza kisasi kwa watu waliomuua Erasto bali wao wanamwachia yote Mungu.
Kuhusu kesi
Katika hatua nyingine, polisi mkoani hapa wanaendelea kuwahoji wafanyabiashara maarufu wa madini ya tanzanite wa mji mdogo wa Mererani wanaodaiwa kuhusika na kifo hicho.
Habari za kipolisi zilieleza kuwa mfanyabiashara mmoja wa madini, kijana ambaye aliibuka ghafla kuwa tajiri mkubwa kutokana na biashara ya madini ya tanzanite, anashikiliwa kwa mahojiano.

No comments:

Post a Comment