MAANDAMANO YA CHADEMA HUKO JIJINI MWANZA

MAANDAMANO ya amani yaliyokuwa yameandaliwa na chama cha demokrasia na 
maendeleo(chadema) yamegeuka shubiri kwa wakazi wa jiji la Mwanza baada 
ya kuibuka mapambano makali baina ya waandamanaji hao na jeshi la polisi
 mkoani Mwanza na kusababisha polisi kutumia nguvu kuwatawanya wafuasi 
wa chama hicho. 
Maandamano hayo ya amani ambayo yalianzia katika eneo la Buzuruga nje 
kidogo ya jiji la Mwanza yalikuw ayakiongozwa na wabunge Highness Kiwia 
wa Ilemela  pamoja na Ezekiel Wenje kuelekea katika viwanja vya 
Furahisha yalilenga kumshinikiza Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Ernest Ndikilo 
kutoa barua zinazodaiwa kuandikwa na ofisi ya Waziri Mkuu Tamisemi 
kuwarejesha madiwani watatu waliotimuliwa katika Manispaa ya Ilemela 
kutokana na kushindwa kuhudhuria vikao vitatu mfululizo. 
Polisi wenye silaha pamoja na askari kanzu walianza kutanda katika eneo 
hilo la Furahisha wakiongozwa na Mkuu wa upelelezi wa makosa ya jinai 
Mkoa wa Mwanza RCO Konyo ambaye alikuwa akitumia gari lenye namba za 
usajili DK 068EXV aina ya Toyota Land Cruiser 
Maandamano hayo ambayo awali yalionekana kana kwamba yangelimalizika 
salama yaliwasili katika viwanja vya Furahisha majira ya saa 5.38 huku 
yakiongozwa na gari la polisi lenye namba za usajili za nchi ya Uganda  
779 UAG likiwa nimesheheni polisi wenye silaha nzito ikiwa ni pamoja na 
mabomu ya machozi na bunduki pamoja na askari kadhaa ambao walikuwa 
katikati ya maandamano hayo. 
Baada ya maandamano hayo kuwasili katika viwanja vya Furahisha kwa 
amani,waandamani hao ambao walikuwa na mabango mbalimbali yaliyosomeka 
kuwa ‘Matata hatutaki uendelee kuwa Meya wa Ilemela rudia kazi yako ya 
awali, na jingine Jaji Sumari tumechoka kuahirisha mara kw amara kesi 
dhidi ya Matata na jingine  lililosomeka kuwa RD Ndikilo tunahitaji 
barua za kurejeshwa kwa madiwani wetu. 
Hata hivyo tofauti na ilivyokuwa imetangazwa kuwa maandamano hayo ya 
amani yangelipokelewa na Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Ernest Ndikilo,hakukuwa 
na kiongozi yoyote wa Serikali ambaye alikuwepo uwanjani hapo kupokea 
maandamano hayo. 
Kufuatia kutoonekana kwa kiongozi yoyote wa Serikali,viongozi wa chadema
 pamoja na wabunge wao walikutana kwa faragha kwa dakika kadhaa kwa 
ajili ya kujua hatima ya maandamano hayo ambapo Mbunge wa Nyamagana 
Ezekiel Wenje alipanda jukwaani saa 6.45 na kuwaeleza maelfu ya 
waandamanaji kuwa wameamua kumtuma Mbunge wa Ilemela Highnes Kiwia 
kwenda ofisini kwa Mkuu wa Mkoa wa Mwanza kuchukua majibu kwa ajili ya 
kuwaletea wananchi walioandamana juu ya hatima ya madiwani hao. 
Hata hivyo saa moja baadae Mbunge huyo alisimama jukwani na wakuwaeleza 
waandamani hao kuwa simu ya Mbunge Kiwia ilikuwa haipatikani hivyo 
kuwataka kuandamana kwenda kwa Mkuu wa mkoa wa Mwanza kujua kulikoni na 
hapo ndipo hali ya hewa ilipochafuka. 
Jeshi la polisi baada ya kuona wandamanaji hao wameanza kuelekea katika 
ofisi za Mkuu wa mkoa liliwataka kutawanyika ambapo waandamanaji hao 
walikaidi ndipo jeshi la polisi lilipoamua kutumia mabomu ya machozi 
kuwatawanya wafuasi hao. 
Vurugu hizo ambazo zilianza majira ya saa 7.30 zilisababisha kufungwa 
kwa baadhi ya barabara kutokana na waandamanji hao kuweka vizuizi vya 
mawe na kuchoma matairi,ambapo pia maduka na ofisi mbalimbali 
zililazimika kufungwa kwa muda kupisha vurugu hizo. 
Baadhi ya wananchi ambao walikuwa wakitumia usafiri wa umma walionekana 
wakishuka kupitia katika madirisha ya magari hayo na kukimbia kwa hofu 
ya kujeruhiwa na mabomu pamoja na mawe ambayo yalikuwa yakirushwa na 
waandamanji hao kwa jeshi la polisi. 
MKUU WA MKOA WA MWANZA ALONGA 
Mkuu wa mkoa wa Mwanza akizungumza na Mbunge Kiwia pamoja na viongozi wa
 chadema ofisini kwake alisema kuwa ameshangazwa na uvumi huo kuwa ofisi
 yake imekalia barua a kurejeshwa kwa madiwani Abubakar 
Kapera(Nyamanoro),Dan Kahungu(Kirumba) pamoja na Marietha 
Chenyenge(Ilemela). 
RC Ndikilo alisema kuwa Serikali imekuwa ikifanya kazi zake kwa 
maandishi na sio kwa kufuata maneno ya mtaani na kueleza kuwa hana barua
 yoyote toka ofisi ya Waziri Mkuu inayomualifu kuhusu kuwarejesha 
madiwani hao baada ya kukata rufaa. 
“Hata Mbunge kuna siku ulinipigia simu ukiniuliza juu ya kuwepo kwa 
barua hizo name nilikujibu kuwa kwa kuwa uko hapo Bungeni Dodoma ambapo 
pia kuna ofisi ya Waziri Mkuu nilikujibu kuwa ni muhimu ukawaona 
viongozi wakuu wa Tamisemi ikiwa ni pamoja na Waziri Mkuu,pia 
nilikushauri kuwa wakupe japo nakala ya barua hiyo”,alisema RC Ndikilo. 
“Lakini cha kushangaza nimekuwa nikisikia maneno ya ajabu kuwa nimeficha
 barua za madiwani hao,ikumbukwe kuwa madiwnai hao hawakukata rufaa 
kwangu bali walikata rufaa ngazi ya juu kabisa,ili kukata mzizi wa 
fitina naomba kati ya tarehe 26 hadi 27 wewe Mbunge pamoja na mimi 
twende TAMISEMI kukutana na viongozi ili kukata mzizi wa fitina na tuje 
tuwaeleze wananchi ukweli uliopo”,alisema RC Ndikilo. 
Kuhusu suala la Meya Henry Matata kutoondolewa madarakani RC Ndikilo 
alisema kuwa hawezi kulizungumzia suala hilo kw akuheshimu mamlaka ya 
mahakama na kuwataka chadema kuvuta subira hadi pale mahakama itakapotoa
 maamuzi yake. 
KAULI YA MBUNGE KIWIA 
Akizungumza katika ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza,Kiwia alisema kuwa 
waliamua kuitisha maandamano hayo kutokana na kuelezwa na Waziri Hawa 
Ghasia kuwa tayari barua hizo zimeishatumwa mkoani Mwanza. 
“Mheshimiwa Mkuu wa mkoa hawa madiwani waliosimamishw ani wawakilishi wa
 wananchi,wamekaa nje kwa miezi saba sasa na uchaguzi wa Meya haukuwa 
halali ndio maana tuliamua kuitisha maandamano kwa ajili ya kuhakikisha 
madiwani hawa wanarejeshwa. 
RPC MANGU 
Akizungumza kwa simu juu ya kutokea kwa vurugu zilizosababisha kupigw 
akwa mabomu ya machozi,Kamanda wa polisi mkoa wa Mwanza Ernest Mangu 
alisema kuwa polisi walifanikiwa kudhibiti vurugu hizo na hadi sasa 
hawezi kusema ni wananchi wangapi ambao walikamatwa kuhusu vurugu hizo. 
WANANCHI WAWALAUMU VIONGOZI NA WANASIASA NA KUWAPONGEZA POLISI. 
Baadhi ya wananchi waliozungumza na Mtanzania juu ya vurugu zilizotokea 
waliwaonyoshea kidole wanasiasa pamoja na viongozi wa mkoa wa Mwanza 
kutokana na kushindwa kusema ukweli juu ya tukio hilo. 
Baadhi walisikika wakisema kuwa kama barua zipo kweli madiwani hao 
wanapaswa kupewa na kama azipo basi walioeneza maneno hayo wachukuliwe 
hatua kali kutokana na uchochezi. 
Wananchi hao pia walilipongeza jeshi la polisi kutokana na kutumia 
busara badala ya nguvu kuhakikisha maandamano hayo yanakuwa ya amani. 
 
  
  
  
  
  
  
  
  
  
  
  
 
 

 
No comments:
Post a Comment