Wamo CCM, CHADEMA
Mbunge wa Nzega (CCM), Dk. Khamis Kigwangallah, amesema amepokea
majina ya wabunge, viongozi wa serikali na wafanyabiashara maarufu
nchini ambao ni mapapa wanaojihusisha na biashara ya dawa za kulevya. Hata
hivyo, Dk. Kigwangallah ambaye amepania kuwataja bungeni watu
wanaojihusisha na biashara hiyo haramu, amesema baada ya kukabidhiwa
majina hayo kutoka kwa wananchi, anafanya uchunguzi na kupata ushahidi
ili kujiridhisha kabla hajachukua hatua ya kuwataja. Miongoni
mwa majina ya wabunge aliyopewa wamo kutoka CCM na Chadema, na
wafanyabiashara maarufu wote wanatoka mkoa wa Dar es Salaam.
“Nawashukru wananchi wamenipa ushirikiano hadi jana wamenikabidhi majina ya watu saba ambao ni wabunge wawili, kiongozi mmoja mwandamizi wa serikali na wafanyabiashara wanne, ambao wote ni mapapa wauza unga na siyo madagaa,” alisema Dk. Kingwangallah. Alisema katika kuhakikisha anatekeleza alichoahidi amemwandikia barua Spika wa Bunge kumuomba atoe maelezo kwa kuwataja majina vigogo wanaojihusisha na dawa za kulevya na kwamba bado anasubiri kujibiwa. Dk. Kigwangallah amekabidhiwa majina hayo siku chache tu baada Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Bunge), William Lukuvi, kulieleza Bunge kuwa kama serikali itaamua kutaja wanaojihusisha na biashara hiyo hakuna atakayesalimika ndani ya bunge kwa sababu pia wamo wabunge wanaotajwa.
No comments:
Post a Comment